Tom Regan: Falsafa ya haki za wanyama
Maoni ya mwisho ya Christian Koeder
Dibaji ya Marly Winckler
Kitabu cha Falsafa
ya Haki za Wanyama (The Philosophy of Animal Rights), kilichoandikwa na Tom
Regan, na kuchapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1989, inaweka katika mfumo
na kusambaza kwa lugha iliyo rahisi zaidi hoja kuu aliyoikuza awali katika
kitabu chake Hoja ya Kutetea Haki za
Wanyama (The Case for Animal Rights
(1983), ambacho ni mojawapo ya kazi zilizo makini zaidi, zenye mshikamano
mkubwa wa kimantiki, na zenye hoja kubwa zaidi katika maadili ya haki za
wanyama. Kazi ya Regan ni sehemu ya mjadala ambao tayari ulikuwa umejengeka,
ambapo kuchapishwa kwa Ukombozi wa
Wanyama (Animal Liberation) na Peter Singer mwaka 1975
kulikuwa hatua muhimu sana ya kihistoria. Hivyo basi, Hoja ya Kutetea Haki
za Wanyama (The Case for Animal Rights) pamoja na muhtasari wake wa baadaye
vilijitokeza katika wakati ambao uwezo wa wanyama kuhisi (animal sentience),
tatizo la mateso, na ukosoaji wa ubaguzi wa spishi (speciesism) tayari vilikuwa vimejengeka kwa
kiwango kikubwa ndani ya uwanja wa falsafa.
Regan anapiga hatua moja mbele zaidi kwa kuunda nadharia ya haki za
wanyama inayojengwa juu ya dhana ya thamani ya asili (inherent
value) na wazo la “wahusika wa maisha” (subjects-of-a-life).
Mtazamo huu hauishii tu kukosoa vitendo vya ukatili wa hali ya juu dhidi ya
wanyama, bali pia unahoji uhalali wa kimaadili wa unyonyaji wa wanyama wenyewe.
Kwa msingi huo, unakataa aina yoyote ya matendo yanayowafanya viumbe hawa kuwa
bidhaa za kufanikisha malengo ya binadamu, badala ya kuwatambua kama viumbe
wenye thamani yao ya ndani inayostahili kuheshimiwa.
Hata hivyo,
zaidi ya miongo mitatu baada ya kuchapishwa kwa kitabu hiki—na miaka hamsini
tangu kuchapishwa kwa Ukombozi wa Wanyama
(Animal Liberation)—tunakabiliwa na mkinzano wa kihistoria unaotia
wasiwasi: kamwe hakujawahi kuzalishwa maarifa mengi kiasi hiki ya kisayansi na
kifalsafa katika nyanja ya maadili ya wanyama, na wakati huohuo kamwe
hakujawahi kuwepo idadi kubwa kiasi hiki ya wanyama wanao nyanyaswa kwa kiwango
kikubwa katika viwanda/mashamba ya ufugaji kama ilivyo leo. Uwazi na maendeleo
ya kinadharia yameongezeka kwa kiwango cha ajabu; hata hivyo, mwamko wa kijamii
na mifumo ya kisiasa imeendelea kubaki nyuma kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa
na maendeleo hayo.
Tangu miaka ya 1970, hoja madhubuti zimeweka msingi imara wa
kuthibitisha kwamba wanyama wana uwezo wa kuhisi (animal sentience), zimebomoa hoja
za ubaguzi wa spishi (speciesism), na zimeonyesha wazi
kutokuwiana kwa kimaadili kwa mifumo inayowafanya viumbe wenye hisia kuwa
bidhaa za kutimiza malengo ya binadamu. Katika kiwango cha kimaarifa na
kifalsafa, uhalali wa kimaadili wa unyanyasaji wa wanyama umeterereshwa kwa
kiwango kikubwa. Hata hivyo, mapinduzi
haya ya kimawazo hayajatafsiriwa kuwa mabadiliko ya kimuundo katika jamii.
Umma kwa ujumla, ingawa sasa ina taarifa
na uelewa zaidi kuhusu masuala ya haki za wanyama, bado kwa kiasi kikubwa
imeendelea kuishi ndani ya mifumo ya kitamaduni na ulaji inayotegemea
unyanyasaji wa wanyama. Hali hiyo pia inaonekana pia miongoni mwa wasomi na
viongozi wa kisiasa, kiuchumi, kisanii na kidini, ambao kwa sehemu kubwa
wameendelea kudumisha desturi zao, mitazamo yao na mahusiano yao ya awali bila
mabadiliko makubwa. Mateso ya wanyama sasa yanaonekana zaidi na yanajulikana
kwa watu wengi, lakini bado hayajawa kipaumbele; yamefahamika zaidi, lakini
hayajawa sehemu ya msingi ya maamuzi na mijadala ya kijamii.
Pengo hili linaweza kuelezwa kwa kiasi
fulani na kuendelea kuwepo kwa ukosefu wa elimu ya maadili kuhusu haki za
wanyama, ambayo bado ni nadra sana hata katika taasisi za elimu ya juu.
Wanafunzi katika vyuo vikuu na vyuo vya kati mara chache hupata mafunzo ya kina
na ufahamu mbadala kuhusu maadili ya wanyama au haki haki zao zinazojengwa
katika misingi ya hoja. Kwa wale wanaomaliza programu hizo—au ambao hawapati
kabisa elimu ya baada ya sekondari—masuala haya hubaki mbali zaidi na uelewa
wao. Nje ya duru maalumu za kitaaluma na za wanaharakati, hoja zinazojengwa juu
ya haki za wanyama kwa kiasi kikubwa hazipo katika vyombo vikuu vya habari na
mijadala ya umma. Hata hivyo, pengo hili
linaonekana kwa nguvu zaidi katika ngazi za taasisi za kisiasa, ambapo,
katika nchi nyingi mabunge na taasisi za kutunga sheria huathiriwa kwa kiasi
kikubwa—na mara nyingi hata kudhibitiwa—na makundi yenye nguvu ya maslahi ya
kiuchumi, hasa sekta ya biashara kilimo (agribusiness) na mfumo mpana wa viwanda kilimo na mifugo (agro-industrial complex). Sekta ambazo uhai wake wa
kiuchumi unategemea moja kwa moja ukandamizaji wa wanyama na huwa na ushawishi
mkubwa katika uchaguzi, uundaji wa ajenda za mabunge, na sera za umma, hali
ambayo huendeleza na kuimarisha pengo kati ya mwamko wa kimaadili na mabadiliko
halisi ya kimuundo katika jamii.
Mpangilio huu
umegeuza mjadala kuhusu haki za wanyama kuwa eneo ambalo karibu ni mwiko
kulijadili, ambapo mapendekezo ya kimaadili hukinzana moja kwa moja na maslahi
ya kiuchumi yaliyokita mizizi, na hivyo kusababisha maendeleo ya polepole na
yasiyoendelevu. Hata mipango kama Jumatatu
Isiyo na Nyama (Meatless Monday), inayohimiza kupunguza
matumizi ya bidhaa zinazotokana na wanyama, hukumbwa na upinzani mkali
usioendana na ukubwa wa pendekezo lenyewe, hasa kwa sababu ya umuhimu wake wa
kiishara na kielimu. Upinzani huu hauwezi kuelezwa kwa athari za haraka za
kimatendo za mpango huo, bali unatokana na ukweli kwamba, hata kama ni kwa siku
moja tu, unavunja mtazamo wa kuuchukulia ukandamizaji wa wanyama kuwa
jambo la kawaida na lisilohojiwa, huku ukionyesha uwezekano halisi wa mifumo
mbadala ya lishe na utamaduni.
Mtindo huu wa
mwitikio na upinzani unadhiirisha ukweli mmoja muhimu: maendeleo ya kimaadili
katika nyanja ya haki za wanyama bado yanategemea zaidi duru maalumu za
kihistoria zinazofungua fursa za mabadiliko kuliko uwepo wa mifumo ya kudumu ya
haki. Duru hizi za kipekee zinapofungwa, hali ya kurudi nyuma au kusimama kwa
maendeleo huwa ndiyo inayotawala. Kile ambacho kingepaswa kuwa sera endelevu ya
umma mara nyingi hugeuka kuwa tukio la muda mfupi tu, na kile ambacho
kingepaswa kutambuliwa kama haki ya msingi mara nyingi hubaki kuwa hatua ya
mpito inayoweza kuondolewa wakati wowote.
Hapa ndipo mvutano unapoibuka ambao hatuwezi kuuepuka. Tom Regan yuko
sahihi katika uchunguzi wake wa maadili; hata hivyo, uzoefu wa kihistoria
unaonyesha kwamba kudai kila kitu kama sharti la kuchukua hatua mara nyingi
husababisha kusonga mbele kidogo sana—au kutokusonga kabisa. Juu ya hili
kunaongezwa jambo linalojirudia katika
harakati za kisiasa na kimaadili: ukosoaji wa ndani usioelekezwa kwa
wapinzani wa nje, ila kwa mipango ya mpito inayotoka ndani ya uwanja wa haki za
wanyama wenyewe. Mbali na kuimarisha sababu ya utetezi wa wanyama, mienendo
kama hiyo huwa inagawanya hata zaidi harakati dhaifu ya kisiasa, ikibadilisha
muunganiko unaowezekana kuwa mgongano wa ndani, kudhoofisha uwezo wa kuchukua
hatua za pamoja, na kupoteza fursa muhimu
za kujenga msingi wa pamoja wa
kuwasaidia wanyama kwa ufanisi.
Kwa kuzingatia hili, swali linakuwa lisiloepukika: je, tunapaswa kujiepusha
na kuchukua hatua kwa sababu tu hatuwezi kufikia kila kitu kwa wakati mmoja?
Kwa Regan, mageuzi ya taratibu huwa yanaongeza muda wa ukosefu wa haki kwa
kuhalalisha miundo ambayo inapaswa kufutwa. Hata hivyo, uzoefu wa kihistoria unaonyesha kuwa kusimamisha au kukana
uhalali wa hatua zinazofaa, zinazopimika na zenye uwezo wa kuleta mabadiliko ya
kisiasa kwa jina la usafi wa dhana bora
kunamaanisha, kwa vitendo, kukubali kuendelea kikamilifu kwa madhara
yale yale yanayodaiwa kupingwa.
Kudumisha lengo
la kutokomeza kabisa matumizi na ukandamizaji wa wanyama kama dira ya kimaadili
ni jambo la msingi. Lakini
kuichukulia dira hiyo na sharti la kuchukua hatua za mara moja kunaweza
kubadili uthabiti wa kimaadili na kuwa kupooza kisiasa. Kati ya
kuukubali udhalimu kama ulivyo na kudai ukomeshwe mara moja, kuna njia ya kati.
Katika njia hiyo—ambayo si kamilifu, inayopingwa, na inayofanyika hatua kwa
hatua—watu hubadilisha tabia zao, na namna wanavyowaona kuwatendea wanyama
huanza kubadilika. Njia hii haipunguzi uzito wa dhuluma ya ukandamizaji wa
wanyama; inatambua tu kuwa hoja sahihi
ya kimaadili haitafsiriwi moja kwa moja kuwa mabadiliko ya kihistoria.
Mabadiliko ya aina hii hutegemea mapambano halisi ya kisiasa. Kudharau nafasi
hii ya mpito hakuharakishi ukombozi wa wanyama; bali kunadumisha tu hali
iliyopo.
Kila mlo usio
na bidhaa zinazotokana na wanyama unaotolewa katika shule za umma si ishara
ndogo isiyo na maana. Ni uzoefu halisi
unaofundisha ladha mpya, unaofanya mbadala kuwa jambo la kawaida, unaobadilisha
marejeo ya kitamaduni, na kupanua upeo wa kile kinachoonekana kuwa
kinawezekana. Hili halichukui nafasi ya kutokomeza ukandamizaji wa wanyama, bali huandaa mazingira ambayo yataufanya
utokomezaji huo usionekane tena kama jambo lisilowezekana kufikiriwa.
Kukataa hatua za mpito zinazofanya kazi kwa jina la njia bora ya kinadharia
kunamaanisha kuwanyima msaada wa moja kwa moja wanyama wanaoteseka sasa
hivi—msimamo ambao kwa kawaida tusingeukubali kama ungehusu dhuluma dhidi ya
binadamu. Viwango hivi viwili vya maadili vinaonyesha uwepo wa upendeleo wa
kibaguzi dhidi ya spishi nyingine na kujitenga na hali halisi wanayoishi
wanyama wenyewe.
Kitabu cha Tom
Regan kinaendelea kuwa mwongozo muhimu wa kimaadili kwa sababu kinaweka wazi
kwamba ukandamizaji wa wanyama ni dhuluma inayopaswa kutokomezwa, si kurekebishwa
tu. Katika dhana ya maadili, uchambuzi wake hauna utata; lakini katika dhana ya
kihistoria na kisiasa, uwazi wa dira ya
maadili hautafsiriwi moja kwa moja kuwa mabadiliko ya kijamii. Kati ya
kuthibitisha kanuni na kubadilisha kwa vitendo mifumo ya kijamii, ni lazima kujenga madaraja, hata kama ni ya muda
na yasiyo kamilifu. Kukataa kujenga hatua hizi za mpito kwa jina la uthabiti wa
maadili kunaweza kulinda ubora wa hoja za kimaadili, lakini hakubadilishi sera
za umma, hakubadilishi desturi za kijamii, wala hakupunguzi mateso ya kweli na
ya haraka ya mabilioni ya wanyama.
Marly Winckler
Florianópolis, Brazil
Januari 2026
Swahili Kiswahili