Tom Regan: Falsafa ya haki za wanyama
Maoni ya mwisho ya Christian Koeder
Haki
za wanyama
Kwangu binafsi,
mtazamo wa Regan unaojengwa juu ya haki ni muhimu sana. Haki za
kimaadili (mawazo na kanuni za maadili) pamoja na haki za kisheria
(zinazolindwa na sheria) hujenga uzio wa ulinzi unaomzunguka kila mtu binafsi.
Wengine hawaruhusiwi kubomoa uzio huo, bila kujali mtu huyo amefanya nini—kama
Regan anavyoeleza katika kitabu chake Empty Cages. Fikiria mtu mwovu
zaidi unayeweza kumfikiria (kwa mfano, Hitler). Kwa mujibu wa haki za binadamu,
ingekuwa ni kosa kumuua. Ndiyo, angepaswa kufungwa gerezani maisha yake yote
ili kulinda usalama wa wengine. Wazo la haki za binadamu—lililoimarishwa baada
ya Vita vya Pili vya Dunia, angalau katika nadharia na mara nyingi pia katika
vitendo—ni msingi muhimu kwa uhai wa ustaarabu wa kisasa. Ninaposema ustaarabu,
ninamaanisha kuishi pamoja kwa amani na kuheshimu kanuni za kidemokrasia:
mijadala, sawa; kutokubaliana, sawa; lakini utekaji nyara, mateso, utumwa,
mauaji ya kiholela, mauaji ya kulipa kisasi, na hukumu za kifo—haya yote:
hapana.
Wazo la haki
za wanyama, kwa maana kwamba linakataa aina zote za kuchinja wanyama na
linadai ulaji wa mboga (vegetarianism) si kama ni tendo la huruma kwa
mtu binafsi pekee bali pia ni dai la kisiasa, limejengwa juu ya msingi wa haki
za binadamu. Kwa maana, haki za wanyama
zinajumuisha haki za binadamu.
Kuna mitazamo
mingine pia inayohusiana na haki za wanyama ambayo inasisitiza kuwaheshimu
wanyama na ulaji wa mboga. Mimi binafsi naiona kuwa haina manufaa makubwa. Kwa
mfano, dhana ya ukombozi wa wanyama (animal liberation) inalenga
kuonyesha kwamba tunapaswa kupinga ukandamizaji na unyanyasaji wa wanyama—si
kwamba (kama rafiki yangu mmoja alivyodhani kwa hofu) tunapaswa kufungua
mabanda yote ya bustani za wanyama na kuwaacha simba na mamba washambulie watu.
Badala yake, “Ukombozi wa wanyama” ni wazo linalolenga mabadiliko ya kijamii.
Aidha, mtazamo
wa nadharia ya utumizi (utilitarianism) ya Peter Singer, uliowasilishwa
katika kitabu chake Ukombozi wa Wanyama (Animal Liberation), unaruhusu
baadhi aina za unyanyasaji wa wanyama ikiwa unyanyasaji huo utazalisha manufaa
kwa idadi kubwa ya wengine. Hili linapingana na dhana ya haki za wanyama. Vivyo
hivyo, wazo la kupinga ubaguzi wa spishi (speciesism), ubaguzi wa
wanyama, kwa sababu ni aina ya dhuluma ni lenye mantiki. Hata hivyo, halitoshi
kwani binadamu au mnyama anaweza kutendewa vibaya, ikiwa hakuna mwenye haki.
Safari kuelekea yasiyojulikana?
Ikiwa umeona hoja za Regan
zinashawishi na umeamua kuunga mkono haki za wanyama, hatua inayofuata kwa
mantiki ni kuwa mlaji wa mboga (vegetarian), au kwa usahihi zaidi, kuwa
mvegani (vegan). Kama watetezi wa haki za wanyama na walaji wa mboga,
tunaingia katika eneo la kipekee. Msingi wetu ni imara. Tunaweza kuwa na
uhakika kwamba lishe ya mboga inaweza kuwa yenye afya na salama. Hata hivyo,
tunatembea katika mipaka ya eneo ambalo limechunguzwa kikamilifu, na wakati
mwingine tunaingia katika eneo ambalo bado halijulikani. Hadi sasa, hakuna nchi
duniani ambayo ni ya walaji wa mboga pekee au ya wavegani pekee. Haki za
wanyama zina ushawishi mkubwa wa kimaadili (kwa watu wengi). Pia zinawezekana kutekelezwa
kisheria, lakini hilo linawezekana tu ikiwa watu wengi wataafikiana nasi. Kwa
hiyo, tunazungumzia mawazo ya kufikirika (utopia) yanayoweza
kutekelezeka; tunajua namna ya kuijenga, lakini bado ni maono ya siku
zijazo.
Ili kubadili mahali tunakoweza kufika, ni
lazima kwanza tutambue tulipo sasa. Ni kana kwamba tunaingia katika eneo
lisilojulikana au “msitu” . Safari hiyo inaweza kuwa ya hatari. Kwa nini? Kwa
sababu mabadiliko ya kijamii huambatana na hatari pamoja na matokeo
yasiyotarajiwa. Hili si tatizo linaloihusu tu harakati za vegan au haki za
wanyama. Ni somo la kusikitisha tulilojifunza kutokana na mapambano ya haki za
kiraia na haki za wanawake.
Hata hivyo, harakati za haki za wanyama zina
upekee wake. Isipokuwa baadhi ya dini zenye kanuni maalumu za lishe, hii ndiyo
harakati ya kwanza ya kijamii inayodai kwamba watu wabadili mfumo wao wa ulaji.
Muhimu zaidi, kwa miongo mingi sasa, mamilioni ya watu tayari wameingia katika
eneo hili “lisilojulikana” la maisha ya vegani. Zaidi ya hayo, eneo hili la
vegani limeendelea kupanuka polepole na kuingia katika maeneo ambayo hapo awali
yalitawaliwa na ulaji wa vyakula vya bidhaa za nyama.
Hata hivyo, makosa mengi yamefanyika, na
mafunzo mengi yamepatikana kutokana na uzoefu huo. Kwa nini tusitumie “maarifa
ya ndani” hayo ili kufanya safari yetu iwe rahisi na yenye mafanikio zaidi?
Inasemekana, na nami nakubaliana na hilo, kwamba kuna maeneo mawili makuu
ambayo mara nyingi husababisha changamoto: (1) lishe na (2) maisha ya
kijamii.
Lishe
Vitabu vya mwanzo vilivyounganisha dhana za haki za wanyama na ulaji wa
mboga vilianza kuchapishwa mwishoni mwa miaka 1800, hasa kitabu cha Henry
Salt, Haki za Wanyama (Animals’
Rights), kilichochapishwa mwaka 1892. Wakati huo, sayansi ya lishe
haikuepo. Vitamini, ambavyo ni muhimu kwa afya ya binadamu, viligunduliwa
katika nusu ya kwanza ya miaka ya 1900. Shirika la kwanza lililojitambulisha
rasmi kama la vegani, yaani The Vegan Society nchini Uingereza,
lilianzishwa mwaka 1944. Vitamini ya mwisho kugunduliwa—vitamini B12—ilitengwa
na kutambuliwa takriban miaka minne baadaye. Hata hivyo, mawazo mengi kuhusu
lishe yaliyopatikana katika vitabu vya kale vya wavegani vya karne ya kumi na
tisa yameendelea kurudiwa ndani ya harakati za wavegani hadi leo.
Wakati huo huo, sayansi ya lishe imegundua changamoto mbalimbali
zinazoweza kujitokeza katika lishe ya vegan pamoja na njia za kuzitatua. Hivyo
basi, tuyatumie maarifa hayo ya kisayansi.
Kama mtaalamu wa sayansi ya lishe na mtu ambaye ameishi maisha ya vegan
kwa muda mrefu, ninapendekeza kanuni zifuatazo. Tunaweza kuziita kanuni sita
za dhahabu za lishe ya vegan:
- Badala
ya bidhaa za wanyama, tumia mikunde na vyakula vya mikunde, kama vile tofu, maziwa ya soya, maharage, dengu (ades), kabuli na
karanga.
- Mikunde
ni chanzo bora cha protini, madini ya chuma (iron), na zinki.
- Tumia
kirutubisho cha vitamini B12,
isipokuwa kama unatumia vyakula vilivyoongezwa vitamini B12 karibu kila
siku.
- Tumia
takribani mikrogramu (µg) 10–50 kwa siku, au µg 2,000 mara moja
kwa wiki.
- Hakikisha
unapata vitamini D ya kutosha,
kupitia kirutubisho (takribani µg 20–25 kwa siku) au kwa kupata
mwanga wa jua wa kutosha.
- Pata
iodini ya kutosha
kupitia chumvi yenye iodini, mwani wa baharini (kama nori au wakame),
au kirutubisho chenye µg 100–150 kwa siku.
- Jaribu
kutumia mara kwa mara vyakula vyenye asidi mafuta ya omega-3, kama vile mafuta ya mbegu za kitani (flaxseed oil), mafuta
ya canola (rapeseed/canola oil), jozi (walnuts), au mbegu za
katani (hempseeds).
- Kula
vyakula vyenye kalsiamu kwa kila siku, kama vile vyakula vilivyoongezwa kalsiamu, sukuma wiki, kabichi
ya Napa (kabeji ya kichina, chainizi, napa cabbage), bok choy, au
broccoli.
Maelezo ya ziada
- Kirutubisho
cha vegan chenye virutubisho vingi (vegan multinutrient supplement)
kinaweza kuwa chaguo rahisi kwa sababu mara nyingi huwa na vitamini
B12, vitamini D na iodini kwa pamoja.
- Vitamini
B12 ndiyo kirutubisho muhimu zaidi. Hata watu wanaokula mboga pamoja na maziwa na mayai (ovo-lacto
vegetarians) mara nyingi wanashauriwa kutumia kirutubisho cha B12.
- Lishe
bora inapaswa kujumuisha matunda mengi, mboga mbalimbali, nafaka
zisizokobolewa (whole grains), mikunde, pamoja na karanga, mbegu na
mafuta yenye afya yatokanayo na mimea.
- Maelezo
zaidi kuhusu lishe ya vegan yanapatikana kupitia International
Vegetarian Union (IVU) na The Vegan Society.
(2) Maisha ya kijamii
Wakati Donald Watson—mtu aliyebuni neno “vegan”—aliulizwa,
“Ni jambo gani unaloliona kuwa gumu zaidi kuhusu kuwa vegan?” alijibu: “Nadhani
ni upande wa maisha ya kijamii.”
Unapokuwa mlaji wa mboga (vegetarian),
na hasa mvegani, unaweza kukutana na changamoto kutoka kwa watu wanaokula
bidhaa za wanyama (omnivores) pamoja na kutoka kwa baadhi ya vegans
wenyewe. Baadhi ya walaji wa bidhaa za wanyama watakuunga mkono. Lakini wengine
wanaweza kukasirikia, kuhisi kuudhiwa, kukerwa, au kujitetea kana kwamba
uchaguzi wako unawakosoa wao. Wengine wanaweza hata kujaribu kuhusisha kila
tatizo dogo la kiafya unalopata na lishe yako ya vegan.
Mnamo mwaka 1944, Donald Watson
aliandika:
“Tunaweza kuwa na uhakika kwamba, ikiwa hata
chunusi moja tu itatokea na kuharibu uzuri wa mwili wetu, dunia itaamini kwamba
hilo limetokana kabisa na kosa letu wenyewe kwa kutokula ‘chakula sahihi’.”
Kukutana na wavegani na watetezi wa haki za
wanyama kunaweza kuwa jambo la kufurahisha sana. Wanaweza kubadilishana uzoefu,
kutoa ushauri, kukutia moyo, na mara nyingi ni watu wenye utu mzuri. Hata
hivyo, ni muhimu kukumbuka kwamba hili ni kundi lenye watu wa aina mbalimbali.
Huenda ukakutana na baadhi ya wavegani ambao mitazamo yao au tabia zao utaziona
kuwa za “kipekee” (kama wanavyosema nchini Uingereza) au hata “zisizopendeza”
(kama tunavyosema nchini Ujerumani).
Kwa asili, wanadamu si rahisi kuelewana nao
kila wakati. Na kuwa mvegani au mtetezi wa haki za wanyama kunaweza kufanya
mahusiano ya kijamii yawe magumu zaidi. Hata hivyo, kufuata kanuni chache za
msingi kunaweza kurahisisha maisha. Tunaweza kuziita kanuni nne za msingi za kudumisha afya njema ya
akili:
- Usihubiri. Mamilioni
ya wavegani wamejaribu kufanya hivyo bila mafanikio makubwa. Badala yake,
fundisha kwa mfano wa maisha yako. Jitahidi kuwa mvegani mwenye furaha, na
tumia uanaharakati wa kirafiki (friendly activism). Epuka
uanaharakati wa kulazimisha au wenye shinikizo (pushy activism).
- Tambua mipaka yako. Omba watu
wakuheshimu, nawe pia waheshimu wengine. Kubaliana kwamba watu wanaweza
kuwa na mitazamo tofauti. Kusingekuwa na maana ya uvumilivu kama mambo
yangekuwa rahisi.
- Jumuika na wavegani wengine. Mara
nyingi wanaweza kukupa msaada na ushauri muhimu. Hata hivyo, usitarajie
wawe wakamilifu au kana kwamba ni jini wa kwenye chupa anayetimiliza kila
unachotamani
- Tunza afya yako. Usiwe
mshupavu wa kupindukia (fanatic). Hakuna jambo lolote maishani
linaloweza kufanywa kwa ukamilifu wa asilimia 100.
Hitimisho ni nini?
Kwa upande wa lishe, lishe ya vegan
inaweza kuwa yenye afya sana, lakini bila shaka kuwa vegan hakumaanishi moja
kwa moja kwamba lishe yako ni bora kiafya. Mambo muhimu zaidi ni kuhakikisha
unapata virutubisho muhimu, hasa vitamini B12, na kwamba, kadiri
inavyowezekana, msingi wa lishe yako uwe vyakula vya asili ambavyo
havijasindikwa sana (whole foods). Swali
ambalo limekuwepo kwa karne nyingi na bado hujitokeza mara kwa mara ni: “Je,
kimaumbile binadamu ni walaji wa vyakula vya mimea na nyama (omnivores)?”
Hata hivyo, kwa mtazamo wa epidemiolojia ya kisasa ya lishe
(yaani tafiti za lishe zinazofanywa kwa binadamu) swali hilo si muhimu sana.
Aidha, ni swali linalorahisisha mno jambo lenyewe. Swali muhimu zaidi ni: Tafiti
zinazowahusu watu wanaofuata lishe ya vegan zinaonyesha nini?
Jibu ni kwamba zinaonyesha kuwa lishe ya vegan inaweza kuwa yenye afya sana.
Kwa upande wa maisha ya kijamii, katika
historia yote haijawahi kuwa rahisi, yenye urahisi, na inayokubalika zaidi
kijamii kuwa mvegani. Kwa maoni yangu,
inaweza kuwa mkakati wenye manufaa kukubali kile ninachokiita “mkinzano
wa kimaadili” (ethical paradox). Kwa
upande mmoja, mtu anaweza kutetea haki za wanyama, kutambua kwamba haki hizo
zinadai ulaji wa mboga, na kwamba ulaji wa mboga ulio thabiti kabisa
unamaanisha kuwa mvegani. Kwa upande mwingine,
unaweza pia kushikilia mtazamo kwamba kila mtu ana haki ya kuchagua aina ya
lishe anayopendelea. Kwa mantiki ya kawaida, msimamo huu unaweza kuonekana kuwa
na mkanganyiko. Unaweza kuonekana kama mtu anayedai haki za wanyama kama suala
la kisiasa, lakini wakati huo huo anavumilia kwa ukarimu ukiukwaji wa haki
hizo. Hata hivyo, huu ni mkakati unaoweza kuwasaidia
walaji wa bidhaa za wanyama (omnivores) kuvumilia
na kukubali mitazamo yako. Hali hiyo inaweza kurahisisha maisha yako na
kukusaidia (kwa kutumia maneno ya Colleen Patrick-Goudreau) kuwa “vegan mwenye furaha” (joyful
vegan). Zaidi ya hayo, mkakati huu unaweza pia
kuwasaidia wanyama, kwa sababu unajenga madaraja yanayoelekea kwenye
kutambuliwa kwa haki za wanyama badala ya kujenga kuta
zinazowatenganisha watu.
Binafsi, ninapendelea mtazamo huu. Sipendi
mitazamo ya kimadhehebu, ya kujinyima kupita kiasi, ya kujitesa, ya kufanya
kazi bila kupumzika, au ya kujiona kama shahidi. Kwa kutumia maneno ya Mephistopheles,
mhusika katika tamthilia Faust ya Johann
Wolfgang von Goethe ya mwanzoni mwa karne ya kumi na tisa: “Mtu
hahitaji kujitesa kwa wasiwasi uliopitiliza.” Cha kufurahisha
ni kwamba maneno haya yanatamkwa na Mephistopheles, mhusika
anayewakilisha aina ya pepo au roho ya ubatili/ukana-maana (nihilism). Ikiwa
hupendezwi na ushauri wa pepo, basi unaweza kufuata ushauri wa Donald
Watson. Alipokuwa na umri wa miaka 94, alipoulizwa kuhusu mafanikio
yake maishani, alisema: “Mimi ni mtu ninayependa kufurahia maisha,
mradi tu sifanyi madhara kwangu mwenyewe, kwa watu wengine, kwa wanyama, au kwa
sayari yetu.”
Dkt. Christian
Koeder
Ellwangen, Ujerumani
Februari 2026
Swahili Kiswahili