Tom Regan: Falsafa ya haki za wanyama - Dibaji ya David Sztybel

 

Tom Regan: Falsafa ya haki za wanyama

Dibaji ya Marly Winckler

Maoni ya mwisho ya Christian Koeder


Dibaji ya David Sztybel

Nimekuwa mvegani na mwanaharakati wa haki za wanyama kwa takribani miaka 37. Nilikuwa na bahati kwamba elimu yangu ya chuo kikuu ilijumuisha masomo ya kazi za Tom Regan. Baadaye, kazi hizo nilizifanyia utafiti wa kina katika tasnifu yangu ya shahada ya uzamivu katika Chuo Kikuu cha Toronto iliyoitwa “Empathy and Rationality in Ethics” (Huruma na Umantiki katika Maadili). Pia nilipata heshima ya kumsikiliza Profesa Regan akitoa mihadhara katika makongamano mbalimbali. Kama ilivyo kwa maandishi yake, kila mara nilipata hisia dhahiri kwamba nilikuwa nikijifunza kutoka kwa mmoja wa wanafalsafa wakubwa kabisa. Ubora wa hali ya juu wa uandishi unaopatikana katika kitini hiki pia unaonekana na kustawi katika vitabu vyake vingi vya kifalsafa, ambapo kazi yake maarufu zaidi ni The Case for Animal Rights (Hoja ya Kutetea Haki za Wanyama). Ninaiheshimu sana kazi yake, lakini pia naihoji, kwa kufuata utamaduni wa falsafa ambao unasisitiza uchambuzi na ukosoaji.

Kitabu hicho kinajikita katika mrengo wanadharia ya kuelezea juu ya haki za mtu binafsi, lakini kinavunja desturi ya muda mrefu iliyokuwa ikichukulia kwa uzito haki za binadamu pekee. Hata hivyo, yeyote anayewachukulia wanyama kwa uzito hawezi kushindwa kuona uzito wa hoja za Regan kuhusu haki za mtu binafsi zinazopatikana pia katika kitini hiki. Regan anasisitiza kwamba maisha ya wanyama yana thamani/umuhimu kwa wao wenyewe, bila kujali manufaa yao ya matumizi kwa wanadamu. Anasema kuwa wanyama wana thamani ya asili na inayojitegemea. Na kwamba wao si bidhaa au rasilimal. Kama anavyoeleza Dk. Regan, kile kinachowatokea wanyama kina umuhimu kwao wenyewe. Aidha, kila mnyama kwa usawa ana maisha ambayo yanaweza kuwa mazuri au mabaya kwake, na kwa sababu hiyo anastahili haki sawa. Kwa msingi huo, Regan anapendekeza kwamba kanuni za haki zipanuliwe ili kuwajumuisha pia wanyama, na kwamba wapewe haki yao ya msingi ya kuheshimiwa – haki ambayo ndiyo msingi wa chimbuko la haki nyingine zote. Msisitizo huu juu ya haki za mtu binafsi bado una umuhimu wa kipekee katika historia na muhimu wake haujapungua, licha ya kuongezeka kwa mitazamo ya kudharau hata haki za binadamu, inaonekana kuongezeka katika masuala mbalimbali ya kimataifa.

Mbali na utetezi wake wa haki za mtu binafsi kwa wanyama, ambao Regan anautetea kwa nguvu na kwa namna ya kukumbukwa, kitini hiki pia kina kile ninachokiita “mawazo yanayostahili kusikika tena na tena” (echoables). Haya ni mawazo na dhamira zinazogusa kwa kina watu wanaochukulia haki na heshima kwa uzito. Ni hoja ambazo Regan alizisisitiza na zinapaswa kuwafanya watu wote kutafakari kwa kina. Wanawake na watu weusi hawapo ili kuwatumikia watu wengine; vivyo hivyo, wanyama hawapo kwa ajili ya kuwatumikia wanadamu. Hakuna mtu mwenye misingi ya kimaadili anayefurahia ubaguzi wa kiholela, chuki zisizo na msingi wa haki, au ubinafsi. Mawazo haya yanagusa mioyo ya wale wote wanaotambua kwamba, hasa katika nyakati hizi ngumu baada ya kifo cha Regan mwaka 2017, tuna wajibu wa kutokukata tamaa kuhusu haki. Kadiri ulimwengu unavyokuwa mgumu zaidi, ndivyo dhamira yetu ya kimaadili inavyopaswa kuwa thabiti zaidi. Ninaamini Regan angekubaliana na kauli hiyo.

Hata hivyo, katika kuandika kitini kinachoitwa “Falsafa ya Haki za Wanyama” hakumaanishi kwamba kazi ya Regan ni kamilifu au kwamba inaweza kutumika bila dosari katika kila wakati na kwa kila hali. Maswali muhimu ya kimaadili bado yapo. Kwa mfano, Regan asingekubaliana na Sheria ya Ustawi wa Wanyama ya Sweden ya mwaka 1988, ambayo ilijaribu kupunguza kwa kiasi kikubwa mateso katika ufugaji wa viwandani wa nguruwe pamoja na mageuzi mengine. Kabla ya sheria hiyo, nguruwe jike hawakuwa wakifungiwa ili kulazimishwa kunyonyesha watoto wao. Lakini sheria mpya ilihitaji kwamba nguruwe wote wawe na uhuru wa kutembea badala ya kufungiwa kwenye vizimba vidogo, wapate majani na malazi yanayofaa, wafugwe kwa makundi badala ya kutengwa, na pia ikakataza kukatwa mikia na meno yao, ingawa utaratibu wa kuwahasi uliendelea kuruhusiwa. Hatua hizi ziliondoa mateso makubwa kwa wanyama. Ni kweli kwamba Sweden haikupiga marufuku kabisa ufugaji wa viwandani. Lakini je, mateso na vifo vya wanyama nchini humo visingepaswa kushughulikiwa kwa namna hiyo, hata kama sheria hiyo ilikuwa na mapungufu? Kwa ujumla, katika mifumo ya ufugaji wa viwandani, vifo vya wanyama ni vingi zaidi. Viwango vya vifo vinaweza kufikia asilimia 15 huku faida za kiuchumi zikiendelea kuongezeka. Tunaweza kuendelea kushikilia lengo la kuanzisha haki za wanyama hadi siku ambayo dunia itakapokuwa tayari kwa hali hiyo. Kwa sasa, ni jambo jema kwa “wale wanyama” wenye bahati wanaolindwa katika makazi ya wanaharakati na vituo vya kuhifadhi wanyama, ambapo wanaishi chini ya ulinzi wa misingi ya haki za wanyama. Lakini ni jambo la kusikitisha kwa “wale wanyama” wasiokuwa na bahati wanaoteseka katika mazingira ya kikatili ya ufugaji wa viwandani.

Katika kitini hiki, Regan anazungumzia umuhimu wa huruma, uwezo wa kujihusisha na hisia za mwingine, na upole. Hata hivyo, kitabu chake The Case for Animal Rights (Hoja ya Kutetea Haki za Wanyama) kinaakisi zaidi kauli nyingine inayopatikana pia katika kitini hiki: “Falsafa ya haki za wanyama inahitaji tu: kwamba mantiki hiyo iheshimiwe.” Katika kazi yake kuu, Regan hatoi uzito mkubwa kwa maadili ya kujali (care), jambo ambalo limekosolewa na baadhi ya wanafalsafa wa kike (feminist philosophers). Inawezekana mtu akakubaliana kwamba hoja za Regan zinaendana kikamilifu na mantiki, lakini wakati huo huo asiwe na hisia zozote za kuwajali wanyama. Hali hiyo ingewanufaisha wanyama kwa kiwango kidogo sana, au hata kutowanufaisha kabisa. Kwa upande mwingine, maadili yanayojengwa juu ya huruma pekee nayo yana matatizo yake. Ikiwa unamwonea huruma mtu mwingine—dhana ambayo ni msingi muhimu katika maadili ya kujali (care ethics)—je, hilo lina thamani gani ikiwa mtu huyo mwenyewe ni fisadi au mkatili? Kwa hiyo, mawazo yanayotegemea mantiki pekee na yale yanayotegemea hisia pekee yote yanaweza kuzaa matatizo ya kimaadili. Swali linalobaki ni hili: Je, tunaweza kujenga falsafa moja inayounganisha kwa usawa mantiki na huruma?

Swali lingine muhimu ni: Ni wanyama gani wanapaswa kujumuishwa katika haki za wanyama? Kwa suala hili, Regan anastahili pongezi nyingi. Anaonyesha busara kwa kutetea haki za mbwa, lakini si haki za viumbe rahisi sana kama amoeba. Hata hivyo, anasisitiza kwa uangalifu kwamba hata maumivu ya viumbe kama konokono wasiokuwa na magamba (slugs) yanapaswa kuzingatiwa. Katika kitabu chake, Regan anafanya juhudi kubwa kutetea msimamo wake kuhusu ni wanyama gani wanaostahili hadhi ya kimaadili. Anawaita viumbe hao “subjects-of-a-life”, aani, viumbe ambao ni wahusika wa maisha (wenye uzoefu wa ulimwengu wao na ambao maisha yao yana umuhimu kwao binafsi). Hata hivyo, bado maswali muhimu hubakia na ya kujiuliza. Lakini je, si jambo la kawaida katika falsafa kwamba kila jibu hufungua nafasi ya kuuliza maswali mapya? Kwa hiyo, tuendelee kuchunguza maswali haya kwa kina, huku tukiwatazama wanyama kwa kuzingatia kile ambacho Regan alikiita kwa uzuri sana “kanuni ya heshima” (the respect principle) katika kitabu chake cha The Case for Animal Rights (Hoja ya Kutetea Haki za Wanyama)

Dk. David Sztybel

Maberly, Ontario, Canada

Januari 2026



Swahili   Kiswahili